Endapo msimamizi wa mirathi amesimamia au ametumia mirathi ya marehemu vibaya, warithi halali wa marehemu, pamoja na mambo mengine, wanaweza kufanya yafuatayo; -Wanaweza kuiomba mahakama kumfutia utekelezaji au usimamizi wa mirathi na hivyo kulazimika kurudisha mahakamani hati zote zilizotolewa na mahakama kuthibitisha utekelezaji au usimamizi wake wa mirathi, ili mahakama iweze kumchagua mtu mwingine. -Kama amekataa kurudisha mahakamani hati zote zilizotolewa na mahakama kuthibitisha utekelezaji au usimamizi wake wa mirathi, warithi wanaweza kumshitaki na akikutwa na hatia anaweza kutozwa faini au kifungo kisichozidi miezi mitatu au vyote faini na kifungo. -Kama mtekelezaji huyo na/au msimamizi wa mirathi amesimamia vibaya au ameharibu mali ya marehemu, warithi au mtu yeyote mwenye maslahi na usimamizi huo, anaweza kumfikisha mahakamani akimtaka alipe fidia kwa uharibifu au hasara aliyosababisha.